Header AD

header ads

Mhe. Mchengerwa: chagueni viongozi watakaowaletea maendeleo wanarufiji




Na John Mapepele

Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo na Mbunge wa Rufiji, Mhe. Mohamed Mchengerwa amewaasa wajumbe wa mkutano mkuu  wa CCM Wilaya ya Rufiji kufanya maamuzi sahihi ya kuwachagua viongozi bora na waadilifu wataowaletea maendeleo ya kweli.


Mhe. Mchengerwa ambaye amekuwa mgeni rasmi kwenye mkutano uliofanyika leo Oktoba 3, 2022 Utete wilayani Rufiji amesema wanarufiji wana kiu ya maendeleo hivyo ni  muhimu kufanya maamuzi sahihi.

"Rufiji tunayoikusudia  ni Ile ya miaka ya 1960 ambayo Rufiji ilikuwa ikiheshimika kwa maendeleo katika nchi yetu" amefafanua Mhe. Mchengerwa


Amefafanua, kuwa katika miaka ya 1960, uchumi wa wananchi wa Rufiji ulikuwa juu huku wilaya hiyo ikiongoza katika kilimo cha pamba nchini na Afrika kwa ujumla  huku shughuli za Uvuvi na Kilimo ziliweza kulisha Sehemu kubwa ya Tanzania.

Ameyataja  maendeleo mengine katika kipindi hicho  kuwa ni wilaya hiyo kuwa na  viwanda mbalimbali, vyakula vya kutosha ambapo amefafanua kuwa  nyakati hizo amekuwa akiziita " Nyakati za Kazi kazi".

Aidha, amesema katika kipindi hiki kifupi kumekuwa na maendeleo makubwa katika sekta za afya, elimu na miundombinu hali ambayo imesaidia kuboresha maisha ya wananchi.


"Ni vizuri tukakumbuka kabla ya uchaguzi hali ilikuwa ngumu,  zaidi ya kata nane  hakukuwa na shule, zahanati na hata umeme lakini leo ninavyosimama hapa kata takribani zote  tumeshaleta huduma hizi muhimu na zilizobaki tutazimaliza katika kipindi kifupi kijacho kulingana na mikakati na mipango tuliyojiwekea" amesisitiza Mhe. Mchengerwa

Ameongeza kuwa tayari zabuni kwa ajili ya kutengeneza barabara kwa kiwango cha lami kutoka Nyamwage  hadi Utete imetangazwa na utekelezaji wake unatarajiwa kufanyika  katika kipindi kifupi inavyowezekana.

Pia katika mkutano huo, Mhe. Mchengerwa ameridhia kukarabati ukumbi wa mikutano wa wilaya na ofisi zote za chama katika kiwango cha kisasa huku akitoa usafiri wa  pikipiki kwenye kata zote, Jumuiya zote na baiskeli  4 kwenye kila tawi ili kusaidia utekelezaji wa kazi za chama.

Katika hatua nyingine Mhe. Mchengerwa amewataka wajumbe wa mkutano huo kutanguliza upendo na mshikamano baina yao ili kujiletea maendeleo.


Mhe. Mchengerwa: chagueni viongozi watakaowaletea maendeleo wanarufiji Mhe. Mchengerwa: chagueni viongozi watakaowaletea maendeleo wanarufiji Reviewed by Fahadi Msuya on October 02, 2022 Rating: 5