Header AD

header ads

WIZARA NA JESHI WAUNDA MIKAKATI YA KUBORESHA MICHEZO KIMATAIFA.




Na John Mapepele


Wizara  ya Utamaduni, Sanaa  na Michezo kwa  kushirikiana na Jeshi la Wananchi wa Tanzania  wameweka  mikakati kabambe ya kushinda kwenye  mashindano ya michezo  yanayokuja  hivi sasa  ili kuendelea kuitangaza Tanzania  kimataifa. 


Katika kikao cha pamoja  baina ya Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara ya Utamaduni Sanaa na Michezo, Saidi Yakubu na ujumbe wa Kurugenzi ya Michezo kutoka Jeshi la Wananchi wa Tanzania  mbali ya kuweka  mikakati ya muda mfupi na muda mrefu wamekubaliana kuanzisha  vituo vya kulea  vipaji vya michezo (Sports Academy) nchini ili kuzalisha  vipaji vya wanamichezo watakaoweza kufanya  vizuri.



Akizungumza kwenye kikao hicho, Kaimu Katibu Mkuu, Bwana Saidi Yakubu amesema kuwa  ni ukweli usiopingika kuwa majeshi  yana hazina kubwa ya vipaji vya  michezo ambavyo kama  vikitumika  vizuri  vitasaidia  kuipeleka nchi katika kiwango cha kimataifa kwenye michezo.


Ameitaja   baadhi ya mikakati  iliyojadiliwa  kuwa ni pamoja na kuwa mpango wa maandalizi wa kushiriki kwenye mashindano ya Olympiki na Mashindano ya Afrika, kuendeleza  miundombinu ya michezo, kuwa na  mashirikiano ya Sports Academy na kuingia  makubaliano ya kisheria(MoU) kwenye michezo baina ya Jeshi na Wizara.

Ameelekeza kufanyika kikao  kujuadili  masuala ya kiufundi ndani ya muda usiopungua siku saba baina ya Wizara na Jeshi ili kuja na mpango wa utekelezaji  wa muda mfupi na mrefu  ili utekelezaji wake uanze mara moja.


Aidha amesema  kikao hicho cha kujadili  mambo ya kiufundi  pia kitajadili namna  bora ya kuwashirikisha wadau mbalimbali wa  michezo ili  kuleta tija  katika mikakati hiyo. 

Mkurugenzi wa Michezo wa Jeshi la Wananchi Tanzania  Kanali Martin Sterwart amemshukuru Kaimu Katibu Mkuu Yakubu kwa mwongozo alioutoa ambapo amemhakikishia kwa  upande wa jeshi watakwenda  kutekeleza  mara moja kwa  faida  ya taifa zima.


WIZARA NA JESHI WAUNDA MIKAKATI YA KUBORESHA MICHEZO KIMATAIFA. WIZARA NA JESHI WAUNDA MIKAKATI YA KUBORESHA MICHEZO KIMATAIFA. Reviewed by Fahadi Msuya on September 13, 2022 Rating: 5